Kuishi Kama Mkristo - Somo la 4: Kusema Uongo

Usomaji wa Maandiko: 2 Wafalme 5:20-27

Mstari wa Kukariri: "Midomo ya uongo ni chukizo kwa Bwana; Bali watendao kweli ndio furaha yake." Mithali 12:22

Utangulizi:

Wakati mmoja mchungaji maarufu, Warren A. Candler, alipokuwa akihubiri hadhira kubwa, alitumia kama maandishi yake hadithi ya Anania na Safira, waliomwambia Mungu uwongo na wakauawa. Askofu mzee alitangaza: “Mungu hawapigi watu wafe kwa kusema uongo kama alivyokuwa akifanya. Kama angefanya hivyo, mimi ningekuwa wapi?” Baada ya kuwaruhusu hadhira yake kutabasamu kwa muda, aliendelea. “Nitawaambia ningekuwa wapi,” alisema kwa sauti kubwa. “Ningekuwa hapa nikihubiria nyumba tupu!”

Bila shaka kutaniko lilinyamaza, kwa sababu kusema uongo ni tatizo kubwa ambalo ulimi wa kila mtu unaonekana kuwa nalo kwa asili. Biblia inazungumzia kwa nguvu sana kuhusu matokeo ya kusema uongo. Pia inatuonyesha faida ya kuwa mkweli na mwaminifu.

Maurice Dametz aliwahi kusimulia hadithi kuhusu wavulana watatu waliofika shuleni wakiwa wamechelewa yapata saa 4:00 asubuhi siku moja. Walikuwa wakivua samaki. Walimwambia mwalimu kwamba walichelewa kwa sababu ya tairi kupasuka. Mwalimu aliamua kuwapa mtihani mara moja, kwa hivyo akawaagiza wakae kando. Alisema, "Mtihani huu utakuwa na swali moja tu, nami nitawapa sekunde thelathini kuandika jibu lenu." Kisha akaandika swali ubaoni, "Tairi gani?" Mwalimu alikuwa na busara sana, matokeo ya mtihani yalionyesha wavulana hao watatu walikuwa wamedanganya.

Tukidanganya, tunaweza kufikiri, kama wavulana hawa watatu, kwamba marafiki na majirani zetu hawatatugundua, lakini uongo wetu haujafichwa kwa Mungu. Labda Mungu atachagua kuzuia (kwa muda) hukumu dhidi yetu kwa uongo wetu. Lakini msidanganyike, Mungu anajua kila neno la uongo tunalosema, naye atatuhukumu.

Maswali ya Somo:

  1. Ni nani baba wa uongo wote? Yohana 8:44.
  2. Bwana anafikiria nini kuhusu ulimi wa uongo? Mithali 12:22.
  3. Shiriki mawazo kadhaa kuhusu mistari hii kuhusu uongo:
    • Zaburi 31:18.
    • Mithali 12:19.
    • Mithali 19:22.
    • Mithali 21:6.
    • Yeremia 7:4, 8.
    • Waefeso 4:25.
  4. Je, kuna nafasi kwa mwongo asiyetubu kufanikiwa katika ufalme? Ufunuo 21:8; Ufunuo 21:27.
  5. Elisha alimuuliza Gehazi swali gani, na jibu lake lilikuwa nini? 2 Wafalme 5:25. Je, Elisha alijua kile Gehazi alikuwa amefanya? 2 Wafalme 5:26.
  6. Nani alidanganya kuhusu kumjua Yesu? Marko 14:66-71. Je, Bwana alijua hili lingetokea? Mathayo 26:34.
  7. Adhabu ya Gehazi kwa kusema uongo ilikuwa ipi? 2 Wafalme 5:27. Kwa nini Petro hakuadhibiwa vivyo hivyo kama vile Gehazi alivyoadhibiwa? Marko 14:72; 1 Yohana 1:9.